Mhe. Bernard K. Membe, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania akimkabidhi Mhe. Yousuf bin Alawi bin Abdulla, Waziri wa Mambo ya Nje wa Oman Ujumbe Maalum kutoka kwa Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenda kwa Mhe. Sultani Qaboos bin Said Al Said, Mtawala wa Oman.
Makabidhiano yakiendelea huku Balozi wa Tanzania nchini Oman, Mhe. Ali Ahmed saleh akishuhudia.
Waziri Membe akiwa kwenye mazungumzo na Mhe. Alawi bin Abdulla, Waziri wa Mambo ya Nje wa Oman.
Mhe. Bernard K. Membe (Mb.) Waziri wa Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa amekabidhi ujumbe maalum kutoka
kwa Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania kwenda kwa Mhe. Sultani Qaboos bin Said Al Said,
Mtawala wa Oman.
Ujumbe huo maalum ulikabidhiwa kwa Mhe. Yousuf bin Alawi bin
Abdulla, Waziri wa Mambo ya Nje na mwenyeji wa ziara ya
Waziri Membe nchini Oman, kwenye ofisi za Wizara hiyo jijini
Muscat, Oman Alhamisi Aprili 16, 2015.
Makabidhiano hayo ya kihistoria nchini hapa, yalishuhudiwa na
Mhe. Dkt. Mwinyihaji Makame, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais
Utawala Bora, Zanzibar , Mhe. Ali Ahmed Saleh, Balozi wa
Tanzania Oman, na viongozi wengine wa nchi zote mbili na
waandishi wa habari.
Baada ya makabidhiano, viongozi hao wawili na ujumbe wao
walitumia fursa hiyo kuzungumzia masuala mbalimbali ya
ushirikiano baina ya Tanzania na Oman.
Viongozi hao waliahidi kukuza uhusiano na utamaduni wa nchi
hizi mbili ambao unafanana kwa sababu za kihistoria. Mhe.
Membe alimuelezea mwenyeji wake nia ya Serikali kujenga Ofisi
za Ubalozi kwenye kiwanja chake hapa Mascut kama sehemu ya
utekelezaji wa mpango wa kuwa na majengo ya Tanzania
kwenye nchi mbalimbali duniani.
Aidha mradi mkubwa wa bandari ya Bagamoyo pia ulizungumzwa
na viongozi hao ambapo Serikali ya Oman ni mojawapo ya mdau
wa mradi huo. Wahusika wengine wa mradi wa Bandari ya
Bagamoyo ni Serikali ya China na Tanzania.
Mhe. Yousuf bin Alawi bin Abdulla, Waziri wa Mambo ya Nje wa
Omani alimuhakikishia mgeni wake ushirikiano wa Serikali yake
kwenye hatua zote hizi muhimu za kuendeleza na kukuza
uhusiano wa muda mrefu wa nchi hizi mbili.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,
Dar es Salaam
17 Aprili 2015
Hii habari haijaeleza ujumbe wenyewe ni wa nini au Raisi amesemaje.
ReplyDelete