Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) imeahidi kufadhili mradi wa Kuongeza Mnyororo wa Thamani wa Mazao ya Chakula ili kuunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Tano za kujenga uchumi wa viwanda na kuinua kipato cha wakulima.

Hayo yamebainishwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Bi. Amina Khamis Shaaban, baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na  Meneja  wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) anayeshughulikia Maendeleo ya Miundombinu Vijijiji, Bw. Olagoke Oladapa, kwenye Mkutano wa Mwaka wa Benki ya Maendeleo ya Afrika- AfDB unaoendelea Jijini Busan- Jamhuri ya Korea Kusini.

Bi. Amina Shaaban anayemwakilisha Waziri wa Fedha na Mipango,  Dkt. Philip Isdor Mpango, katika Mkutano huo, alisema kuwa mwanzoni mwa mwezi Mei, 2018, AfDB ilituma timu ya wataalam nchini  Tanzania kufanya mazungumzo ya awali na Serikali kuhusu utekelezaji wa mradi huo ambao ni ahadi ya  Rais wa AfDB, Dkt. Akinumwi Adesina kwa Mhe. Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli wakati wa  ziara yake ya  kikazi nchini Tanzania mwishoni wa mwezi Aprili, 2018.

Miongoni mwa viongozi wa Serikali waliokutana nao ni pamoja Mawaziri kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, na Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

“Serikali imefurahishwa na utayari wa AfDB kufadhili mradi huo kwani utachangia ukuaji wa uchumi na kuleta maendeleo katika sekta ya viwanda na kilimo nchini Tanzania” alisema Bi. Shaaban

Naibu Katibu Mkuu Bi. Shaaban alisema utekelezwaji wa mradi wa kuongeza mnyororo wa thamani ya mazao ya chakula utanufaisha watu wengi hasa wa kipato cha chini kwa kuwa sekta ya kilimo Tanzania inachukua nafasi kubwa katika kuinua uchumi wa nchi.

Aidha, Naibu Katibu Mkuu, aliahidi kuwa Serikali itaharakisha ukamilishaji wa taratibu za maandalizi ya awali ya mradi huo utakao chochea maendeleo ya Sekta ya Kilimo na Viwanda kwa kiasi kikubwa kwa kuwa tayari Benki ya AfDB imeonesha utayari wa kuupatia fedha.  
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Bi. Amina Khamis. Shaaban (kushoto) akiwa kwenye mazungumzo na Meneja wa Benki ya Maendeleo ya Afrika- AfDB anayeshughulikia Maendeleo ya Miundombinu Vijijiji Bw. Olagoke Oladapa (katikati), kuhusu utekelezaji wa mradi wa Kuongeza Mnyororo wa Thamani wa Mazao ya Chakula  Jijini Busan- Korea Kusini.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha na Mipango)

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...